Ticker

6/recent/ticker-posts

Taratibu za amri za ukamataji kwa wakuu wa mikoa.



Kwa MUJIBU wa sheria ya tawala za mikoa, kifungu cha 7, wakuu wa mikoa wanaruhusiwa na sheria kuamuru kukamatwa kwa watu ambao pengine mkuu wa mkoa ana ufahamu kwamba wametenda jinai au wanaweza kutenda jinai au kuvuruga amani mbele yake. Sheria imeweka vigezo na hatua mbalimbali ambazo zinatakiwa kuzingatiwa wakati wa ukamataji kupitia mamlaka ya mkuu wa mkoa kama ifuatavyo;


1. Amri za ukamataji ni katika makosa ya jinai tu na sio madai. (KIF: 7(1) )

2. Mtu aliyekamatwa chini ya amri ya mkuu wa mkoa ni lazima apelekwe mahakamani ndani ya saa 48 tangu kuwekwa kwake kizuizini. (KIF : 7(4) )

3. Endapo saa 48 zikipita bila mtu huyo kupelekwa mahakamani, anapaswa kuachiwa huru na polisi hawataruhusiwa Tena kumkamata mtu huyo chini ya amri ile ile iliyotolewa na mkuu wa mkoa katika kosa lile lile. ( KIF : 7(4) )

4. Mkuu wa mkoa anapotoa amri hii ya kuwekwa kizuizini kwa mtu, anapaswa kuandika katika maandishi sababu za kutoa amri ya kukamatwa kwa mtu huyo na kuzipeleka kwa hakimu au kufanya taarifa hizo zipelekwe kwa hakimu mwenye mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo. Taarifa hizo zinapaswa kupelekwa kwa hakimu wakati wa kumpeleka mahabusu mahakamani. (KIF : 7(5) )

5. Endapo mtu aliyekamatwa na kuwekwa kizuizini ataachiwa kituo cha polisi kabla ya kupelekwa mahakamani, taarifa zake na sababu ya kukamatwa kwake zinapaswa kuwasilishwa kwa hakimu ndani ya muda mfupi baada ya kuachiwa kwa mtu huyo. ( KIF : 7(5) )

6. Endapo mahabusu huyo hakuachiwa kituo cha polisi na  amepelekwa mahakamani, hakimu amepewa mamlaka ya kumweka kizuizini mpaka kukamilika kwa uhakiki wa taarifa kuhusu ukweli wa sababu zilizopelekea mahabusu huyo kukamatwa na kuwekwa kizuizini, pamoja na ushahidi unaoweza kuthibitisha kosa la mahabusu kama ilivyotajwa na kifungu cha 79 cha Sheria ya mwenendo wa mashauri ya jinai SURA 20 iliyorekebishwa 2022.

7. Taratibu zote zingine za kijinai zitaendelea kama inavyoelekezwa na sheria ya mwenendo wa mashauri ya jinai tajwa hapo juu.

Imeandikwa na Johnson Yesaya Mgelwa wa Jungu La Sheria Tanzania.

Chapisha Maoni

0 Maoni